NA HAJI NASSOR, PEMBA
MSAKO wa kawaida kwa wananchi na wakulima, wanaozihifadhi
majumbani karafuu kavu kinyume na sheria, ulifanyika ghalfa, kwenye shehia ya
Msuka wilaya ya Micheweni, ukiongozwa na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa wa
Kaskazini Pemba.
Akizungumza
mara baada ya kumalizika msako huo, ambao haukubaini kuwepo kwa karafuu hizo,
Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama mkoani humo, Omar Khamis Othman
alisema hilo ni zoezi la kawaida.
Alisema
zoezi hilo halimlengi mtu mmoja, bali kila kamati inapoona inafaa na kwa shehia
nyengine, humuarifu sheha wa shehia husika na kulifanya, ili kujiridhisha.
Alisema
wananchi watakaobahatika kupitiwa na zoezi hilo, wasiwe na wasiwasi wala
kujisikia vibaya, kwani ni sehemu ya kazi ya kamati ya ulinzi na usalama.
Mwenyekiti
huyo wa kamati ya ulinzi ambae pia ni Mkuu wa Mkoa wa kaskazini Pemba, alisema
kwa vile ni kinyume kuzihifadhi karafuu kavu ndani bila ya kuwa na nyaraka
kutoka ZSTC, ndio maana kila wanapopata taarifa, huamua kujiridhisha.
“Msako
huu hauna lengo la kumdhalilisha mwanchi yeyote, kwani ni sehemu ya kazi yetu
kama walinzi wa wananchi na mali zao, maana pamoja na kwamba ni kosa kukaa na
karafuu, lakini pia ni hatari kwa mwenye nyumba”,a lieleza.
Katika
hatua nyengine Mkuu huyo wa Mkoa, alisema zoezi kama hilo walilifanya hivi
karibuni shehia za Mtambwe na kukamata idadi kubwa ya gunia za karafuu, ambapo
linalofuata ikiwa mmiliki huyo mali ni yake, huuzwa na kupewa fedha zake.
Kamanda
wa Polisi Mkoa huo, Haji Issa Haji, alisema msako wa karafuu nyumba hadi
nyumba, utafanyia kila wanapopokea taarifa za kuwepo kwenye shehia mbali mbali.
Kamanda
huyo, aliwataka wananchi na viongozi wa shehia, kutoa ushirikiano wa hali ya
juu, maana wapo wananchi wasiokuwa wema, huzitorosha kimagendo karafauu hizo.
Mdhamini
wa Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na uhujumu wa uchumi ZAECA, Pemba, Suleiman Ame
Juma, alisema ili zoezi kama hilo na jengine lifanikiwe, lazima wananchi washirikiane
na taasisi nyengine.
“Sisi
ZAECA na hata Polisi, tunahitaji ushirikiano na wananchi tena hasa wa kawaida
kutoa taarifa kwetu, ili sisi tuangalie sheria zinasemaje”,alieleza.
Baadhi
ya wananchi waliofanyiwa upekuzi huo, walisema wanashukuru kamati hiyo ya
ulinzi na usalama, kutokana na kuwasafisha kwao na hata kwa wananchi wenzao.
Abdalla
Ali Said (65), alisema sasa ameshatoka wasiwasi ambao pengine wananchi
waliokuwa nao au hata serikalini, kutokana na kuhifadhi karafuu kinyume na
sheria, jambo ambalo sio sahihi .
Nae
Salma Said Salim, alisema mume wake ni kweli amekodi mikarafuu wilaya ya
Chakechake, lakini amekuwa akiuza kila wiki mara moja na wala hajawahi
kuhifadhi karafuu ndani mwake.
“Kama
mnawasiwasi wa karafuu, Sheha piteni na watu wako mtafute, lakini humu hata za
dawa hazimo, maana mume wangu anatabia kila mwisho wa wiki anaunza
ZSTC”,alisema.
0 comments:
Post a Comment