Kwa habari za kijamii, kisiasa, kiuchumi na kiburudani



Kwa habari za kijamii, kisiasa, kiuchumi na kiburudani

Labels

Sunday, November 26, 2017

WATOTO 20 WENYE MATATIZO YA MOYO WAFANYIWA UPASUAJI WA BILA KUFUNGUA KIFUA.


israel
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na Taasisi ya Okoa Moyo wa Mtoto (Save a Child Heart – SACH) ya nchini Israel wamefanya upasuaji  wa bila kufungua kifua (Catheterization) kwa watoto 20 wenye matatizo ya Moyo.

Upasuaji huo ambao unatumia mtambo wa Cathlab umefanyika katika kambi maalum ya matibabu iliyoanza tarehe 23/11/2017 na kumalizika kesho tarehe 27/11/2017. Matibabu yaliyofanyika ni ya kuziba matundu kwenye moyo na kutanua mishipa ya moyo.

Katika kambi hii tunatarajia kufanya uchunguzi wa moyo kwa watoto 100 kati ya hao watoto 60 ambao watakuwa na matatizo makubwa watapelekwa nchini Israel kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji wa kufungua kifua mwakani  na watoto 40 watatibiwa hapa nchini.

Tumepanga kufanya matibabu kwa watoto 25 tunaamini hadi kambi itakapomalizika watoto wote hawa watakuwa wamepata matibabu. Watoto 20 waliopata matibabu wengine wameruhusiwa na waliobaki hali zao zinaendelea vizuri na wataruhusiwa pindi afya zao  zitakapoimarika.

Tangu mwaka 2015 Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete ilianza kushirikiana na Taasisi ya Okoa Moyo wa Mtoto (Save a Child Heart- SACH) ya nchini Israel ambapo hadi sasa jumla ya watoto 40 wamefanyiwa upasuaji wa moyo nchini Israel. Gharama za matibabu ya watoto hawa zinagharamiwa na Taasisi hii. 

Tunawashukuru sana wenzetu hawa wa SACH kwa kuona umuhimu wa kutoa huduma ya matibabu bure kwa watoto wenye matatizo ya moyo. Watoto waliotibiwa wamepona na wale ambao walikuwa wanafunzi   wanaendelea na masomo yao.

Wakati kambi hii inaendelea  baadhi ya wafanyakazi wa SACH na JKCI walienda mkoani Kagera kufuatilia maendeleo ya mtoto Julius Kaijage (12) mwanafunzi wa darasa la nne katika shule ya msingi Green Acres iliyoko Bunazi ambaye alifanyiwa upasuaji wa moyo nchini Israel mwaka 2013. Tumekuwa na tabia ya kufuatilia maendeleo ya watoto tunaowafanyia upasuaji hii inatusaidia sana kufahamu maendeleo yao.

Aidha tunatarajia kuwa na kambi nyingine  ya matibabu ya moyo  kwa watoto  na watu wazima  itakayoanza kesho tarehe 27/11/2017 hadi tarehe 01/12/2017. Katika kambi hii ambayo tutashirikiana na wenzetu kutoka Taasisi ya Open Heart International ya nchini Australia tunatarajia kufanya upasuaji wa kufungua kifua kwa watoto 13 na watu wazima 10.

Tunawaomba wananchi waendeleee kuchangia damu kwani wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji wa moyo wanahitaji kuongezewa damu  wakati wanapatiwa  matibabu. Kwa mtu mmoja mmoja au kikundi cha watu wanaopenda  kuchangia damu tunawaomba  wafike Taasisi ya Moyo iliyopo Muhimbili mkabala na Maabara kuu. Kwa maelezo zaidi wawasiliane kwa simu namba 022-2151379 au 0713304149.

Kama mnavyofahamu matibabu ya moyo ni ya gharama hivyo basi tunaendelea kuwahimiza wananchi  kujiunga na mfuko wa taifa wa bima ya afya ambao utawasaidia kulipa gharama za matibabu pindi  watakapougua na kuhitaji kupata matibabu.

 Kwa namna ya kipekee Bodi ya Udhamini, Uongozi na Wafanyakazi wote wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete tunamshukuru sana Mhe. Rais John Pombe Magufuli katika hotuba yake aliyoitoa tarehe 25/11/2017 wakati wa ufunguzi wa Hospitali ya Taaluma na Tiba ya chuo kikuu cha Afya na Sayansi shirikishi Muhimbili kampasi ya Mloganzila kwa  kutupatia jengo ambalo tutalifanya kuwa jengo la  watoto. 

 Kama mnavyofahamu asilimia 70 ya wagonjwa tunaowafanyia upasuaji wa kufungua kifua ni watoto,  tuna jumla ya vitanda 123 kati ya hivi vitanda vya watoto ni 24 tu. 

 Kuwa na jengo la watoto  kutasaidia watoto kupata sehemu nzuri ya matibabu pamoja na sehemu ya kujifunza mambo mbalimbali kwani watoto wanahitaji kucheza na kujifunza. Watoto wengine wanakaa wodini muda mrefu wakisubiri matibabu, watoto hawa  wakiwa na mahali pa kujifunzia wataweza hata kujifunza kusoma na kuandika.

0 comments:

Post a Comment