Kwa habari za kijamii, kisiasa, kiuchumi na kiburudani



Kwa habari za kijamii, kisiasa, kiuchumi na kiburudani

Labels

Monday, December 18, 2017

Kinana kuendelea kuwa katibu mkuu wa CCM.

Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) nchini Tanzania Abdurahman Kinana ataendelea kuwa katibu mkuu wa chama hicho.

Taarifa kwamba ataendelea kuhudumu zimepokelewa kwa shangwe na vigelegele na wajumbe wanaohudhuria mkutano mkuu wa tisa wa chama hicho mjini Dodoma.

Rais Magufuli ambae ndiye mwenyekiti wa sasa, alitangaza uamuzi huo wa Bw Kinana kwa wajumbe hao takriban 1,900.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Dkt Magufuli alimshukuru katibu mkuu wake na kusema ana imani naye katika utendaji wake wa kazi.

Punde tu baada ya kauli hiyo kutolewa, wajumbe takriban wote walisimama huku wakipiga makofi na wengine wakisema, "Jembe, Jembe."

Bw Kinana ambaye amekuwa akishikilia wadhifa huko tangu serikali ya awamu ya nne, na wachambuzi wamekuwa wakimuona kama kiungo muhimu sana katika kuleta mabadiliko ndani ya Chama.

Awali kulikuwa na tetesi kwamba Kinana angeachia nafasi hiyo kwa lengo la kutaka kustaafu.

Kinana, mbali ya kuwa mwanajeshi mstaafu, ana uzoefu mkubwa katika masuala ya utawala na siasa.

Mambo muhimu mkutano Mkuu wa 9 wa CCM

Unahudhuriwa na wajumbe 1856 sawa na asimilia 99.1

Huu ni mkutano mkuu wa taifa wa kwanza kwa Rais Magufuli tangu kuwa rais.

Uchaguzi wa viongozi unafanyika kila baada ya miaka mitano.

Ni katika uchaguzi huu ambapo viongozi wakuu wa Chama wanachaguliwa, nao ni, mwenyekiti, na makamu wake 2 kutoka bara na Zanzibar.

Aidhaa kunafanyika uchaguzi wa wajumbe wa Halmashauri kuu ya taifa ambapo wajumbe 30 wanatakiwa kuchaguliwa kutoka bara na Zanzibar kati ya makada 690 waliojitokeza kuwania nafasi hizo.

0 comments:

Post a Comment