Waziri wa Madini, Angellah
Kairuki (kushoto) na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo(kulia)
wakifuatilia maelezo yaliyokuwa yanatolewa na Kaimu Katibu Mkuu wa
iliyokuwa Wizara ya Nishati na Madini, Profesa James Mdoe (hayupo
pichani)
Greyson Mwase na Asteria Muhozya
Waziri wa Madini, Angellah
Kairuki ameeleza vipaumbele vyake katika Wizara kuwa ni pamoja na
udhibiti wa utoroshaji wa madini nchini, maslahi kwa wafanyakazi huku
akiwataka watumishi kufanya kazi kwa uadilifu na weledi wa hali ya juu.
Kairuki ameyasema hayo mapema leo
tarehe 10 Oktoba, 2017 jijini Dar es Salaam alipozungumza na
watumishi wa Wizara ya Madini pamoja na taasisi zake, waliopo Dar es
Salaam na Makao Makuu ya Wizara Dodoma. Lengo La kikao hicho lilikuwa
ni kufahamiana na kupanga mikakati ya kushirikiana ili kuhakikisha kuwa
Sekta ya Madini inakuwa na mchango mkubwa katika ukuaji wa Uchumi wa
nchi.
Taasisi zilizoshiriki katika
kikao hicho ni pamoja na Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST), Shirika la
Madini la Taifa (STAMICO), Chuo cha Madini Dodoma (MRI) pamoja na
Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini na Mpango wa Kuongeza
Uwazi na Uwajibikaji katika Tasnia ya Uziduaji (TEITI).
Amesema kuwa Sekta ya Madini
inatarajiwa kuwa na mchango mkubwa wa ukuaji wa uchumi wa nchi na
kuwataka wataalam wa madini kubuni mbinu za ukusanyaji wa maduhuli
pamoja na kuboresha mazingira ya uwekezaji kwenye uchimbaji madini.
Katika hatua nyingine aliwataka
wataalam hao kubuni mikakati ya kuzuia utoroshaji wa madini nchini ili
nchi ipate mapato stahiki.
Amewataka watumishi kuepuka
kufanya kazi kwa mazoea na kuwa wabunifu ili sekta hiyo iwe na mchango
mkubwa kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi.
Naye Naibu Waziri wa Madini,
Stanslaus Nyongo amewakumbusha watumishi kuzingatia Dira na Dhima ya
Wizara ikiwemo kufanya kazi kwa tija ili hatimaye sekta ya madini
iweze kuchangia katika uchumi wa nchi kwa kuwa mchango wa sekta husika
bado ni kidogo.
0 comments:
Post a Comment