Kwa habari za kijamii, kisiasa, kiuchumi na kiburudani



Kwa habari za kijamii, kisiasa, kiuchumi na kiburudani

Labels

Wednesday, October 11, 2017

SUALA LA MIMBA KWA WANAFUNZI KUTUA EAC.


Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki (Chadema), Pamela Massay ameamua kujitolea kusukuma katika bunge hilo hoja ya mtoto wa kike anayejifungua wakati anasoma katika shule za msingi na sekondari aweze kuendelea na masomo yake.

Pamela anaona kwamba iwapo ataiwasilisha hoja hiyo katika chombo hicho cha kutunga sheria cha nchi za Afrika Mashariki na ikapita, itasaidia kumaliza mjadala baina ya wale wanaopinga mtoto huyo asiruhusiwe kuendelea na wanaoiunga mkono.
Hoja hiyo ambayo imekuwa ikiibuka na kupoa, hivi karibuni ilisababisha mjadala uliochukua muda mrefu lakini baadaye ulifungwa na msimamo wa Rais John Magufuli.
Hata hivyo, Juni 22 akiwa ziarani mkoani Pwani, Rais Magufuli alisema katika uongozi wake hakuna mtoto wa kike atakayebeba mimba akiwa shuleni ambaye ataruhusiwa kurejea kuendelea na masomo.
Hata baada ya kauli ya Rais baadhi ya asasi za kiraia na mashirika yanayotetea masuala ya jinsia na haki za binadamu yaliendelea kutoa mapendekezo mbalimbali lakini msimamo wa Serikali haukulegezwa.
Katika hafla fupi ya maadhimisho ya siku ya mtoto wa kike duniani iliyoandaliwa na Taasisi ya Health Promotion Tanzania jana, Pamela alisema kama kijana aliyepitia changamoto nyingi akiwa mwanafunzi, atahakikisha suala hilo linafika katika Bunge la Afrika Mashariki ili liundiwe mapendekezo ya kikanda.
“Kuzuia watoto kurudi shule baada ya kujifungua ni lazima kwanza uhakikishe umewaondolea vikwazo vyote vinavyosababisha mimba hizo, bila kutatua changamoto za kimazingira zinazowakabili na kuwapatia elimu ya kutosha ukiwazuia ni kutowatendea haki,” alisema.
Mbunge huyo alisisitiza kuwa pindi bunge litakapoanza vikao vyake atatumia kamati ya jinsia na vijana kuhamasisha kujadiliwa kwa hoja hiyo kwa ajili ya kupata mwafaka kwa Watanzania na wana jumuiya kwa ujumla.
Kwa upande wake, meneja wa mradi wa utetezi wa Health Promotion, Greysmo Mutashobya alisema takwimu zinaonyesha asilimia 18 ya Watanzania ni watoto wa kike wenye umri wa kati ya miaka 10 hadi 19 hivyo kundi hilo linatakiwa kupata huduma bora ya elimu.
“Serikali inapaswa kutengeneza mazingira ya usawa ambayo yataweza kuhamasisha elimu kwa mtoto wa kike sanjari na kuondoa vizuizi vilivyoko mbele yake katika kuipata elimu hiyo,” alisema Mutashobya.     @MCL

0 comments:

Post a Comment